NEWS

29 Septemba 2019

Waziri Mkuu Aagiza Viongozi Hawa Kukamatwa


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, ameagiza kukamatwa na kuwekwa ndani viongozi wa Kamati ya Watumiaji Maji wa mradi wa maji wa Matunguru uliopo katika Kijiji cha Tungamalenga, wilayani Iringa kwa tuhuma za ubadhilifu wa sh. milioni saba.


Waziri Mkuu ametoa agizo hilo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi, wakati akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Idodi wilayani Iringa.

Waziri Mkuu alimuagiza Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela afuatilie suala hilo kwa kuwa kamati nyingi za watumiaji maji zimekuwa na tuhuma za matumizi mabaya ya fedha zinazokusanywa kutoka kwa wananchi jambo ambalo si sahihi.

Alisema ifikapo saa 4.00 asubuhi ya leo watuhumiwa wote wanaohusika na ubadhilifu huo wawe wameshakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya dola kwa ajili ya kwenda kujibu tuhuma zinazowakabili.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alisema kwamba Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Iringa hadi Ruaha yenye urefu wa kilomita 104 ili kuboresha huduma za usafiri kwa wakazi wa maeneo hayo na kuinua uchumi.