NEWS

1 Oktoba 2019

Kigogo CUF atimkia CCM

Mwanachama Mkongwe wa Chama cha Wananchi (CUF) aliyekuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Singo Kata ya Gongoni katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, Hamisi Mwami (53) amekihama chama hicho na kujiunga CCM.

Mwami ambaye amekuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa huo kwa miaka 20 sasa amesema kuwa ameamua kuhamia CCM kwa utashi wake mwenyewe baada ya kusoma alama za nyakati na kuridhika na utendaji wa Rais John Magufuli.

“Nimesoma alama za nyakati, upinzani hauna la kusema sasa hivi ndio maana nimeamua kuhamia CCM kwa utashi wangu na sio kwa kununuliwa au kushawishiwa na mtu kwani nina uzoefu wa zaidi ya miaka 20 katika siasa sasa nimekuwa kiongozi wa Serikali hivyo nina upeo wa kuona mbali”, amesema.

Aidha amesema uroho wa madaraka unaokitafuna chama cha CUF na vyama vingine vya upinzani ni miongoni mwa mambo ambayo yamedhoofisha upinzani hapa nchini na hivyo kushindwa kuwa watetezi wa wananchi,  ndiyo maana ameamua kujiunga na timu ya watu makini wanaojali sana maslahi ya wananchi.

Mwami amepinga wanaodai kuwa amenunuliwa na CCM akihoji kwa nini hawakudai amenunuliwa na CUF kipindi alipojiunga nao ambapo alisisitiza kuwa aliingia na kuondoka kwa utashi wake na hivi sasa ameamua kuingia CCM kwa utashi wake pasipo kushawishiwa na mtu.