NEWS

7 Juni 2017

UCHAMBUZI KIVUKO CHA MV KAZI: JPM aliahidi, anatekeleza

Na Benjamin Sawe.

Upo usemi wa wahenga usemao “mnyonge mnyongeni ila haki yake mpeni.” Hivi ndivyo ninavyoweza kusema kuhusiana na harakati za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli katika kuhakikisha kuwa Sekta ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi inaimarika.

Dkt. John Pombe Magufuli kabla ya kuteuliwa kuwa Rais, amekuwa Waziri katika Awamu mbili zilizopita. Anao uzoefu mkubwa wa utendaji kazi lakini pia katika kuongoza Wizara ambapo amewahi kuwa  Waziri wa Ujenzi na Miundombinu na Kilimo na Ufugaji. 
Kutokana na umuhimu wa Sekta ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi katika maendeleo ya Taifa, mara tu baada ya kuchaguliwa kuwa Rais, aliagiza ujenzi wa barabara ya kutoka Mwenge hadi Moroco ambayo ilikuwa ina msongamano mkubwa wa magari kuelekea katikati ya jiji.

Msongamano huo umekuwa ukiathiri malengo ya Wafanyakazi ambao walikuwa wakitumia muda mwingi wakiwa kwenye foleni na hivyo kupunguza muda wa kufanya kazi lakini pia uzalishaji na utoaji huduma za msingi kwa Taifa.

Aidha, Mheshimiwa Rais ameshiriki uwekaji wa jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa barabara za juu (fly over) katika makutano ya barabara ya Nyerere na Mandela eneo la Tazara unaogharimu kiasi cha shilingi bilioni 100 za Kitanzania na pia ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma eneo la Ubungo Jijini Dar es Salaam
Hivi karibuni Serikali kupitia Waziri Mwenye dhamana ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa amepokea Kivuko cha MV Kazi ambacho kimejengwa na Kampuni ya Kizalendo ya M/S Songoro Marine Transport Boatyard ya Mwanza.