NEWS

28 Septemba 2019

Siri ya Ukimya wa Joshua Nassari



Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA, Kanda ya Kaskazini, kimeeleza chama hicho bado kinashirikiana na aliyekuwa Mbunge wake wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari, na kueleza wala hakijamtenga kwa kuwa alivuliwa Ubunge.


Kauli hiyo ya CHADEMA imetolewa na Katibu wa CHADEMA Mkoa wa Arusha Elisa Mungure, wakati akizungumza na EATV na EA Radio Digital ambayo ilitaka kujua siri ya ukimya ya Joshua Nassari, na tangu alipovuliwa Ubunge na Spika Job Ndugai.

Katibu wa CHADEMA Arusha Elisa Mungure amesema "siri ya ukimya wa Nassari ni kwamba unapokuwa Mbunge unapata nafasi ya kuzungumza na vyombo vya habari na kufanya shughuli za maendeleo kwenye jamii, na anaonekana akipiga kelele hiyo fursa hana baada ya kunyanganywa Ubunge wake,  amekuwa mwanachama wa kawaida ndani ya CHADEMA, ndiyo maana amekuwa kimya"

"Kuhusu kumtenga hizo taarifa ni za kupikwa unawezaje kumtenga mwanchama kama Nassari, na kama kuna mambo ambayo tunahitaji uzoefu wake huwa tunamuita na anatupa ushauri wake" ameongeza Katibu wa CHADEMA Mkoa wa Arusha Elisa Mungure

Marchi 2019 Spika Ndugai alitangaza kumvua Ubunge Joshua Nassari kwa kushindwa vikao vitatu vya mahudhurio ndani ya Bunge.