“Nataka kusema, wakati ambapo heshima zimekuwa zikimwagwa kwa mashujaa wa Afrika, mtu anayeonewa ni Mwalimu Julius Nyerere,” alisema Mugabe. “Hapa tulipo, vuguvugu za ukombozi, kule tulikokuwepo – tulitegemea msaada wa Tanzania. Lakini hakuna kinachosemwa kuhusu mtu huyu na nchi yake kwenye Jumuiya ya Afrika.”
Mugabe ambaye ni makamu mwenyekiti wa AU, alisema bara la Afrika linapaswa kukumbushwa fadhila inazotakiwa kumlipa Mwalimu Nyerere.
“Nataka sisi Wazimbabwe, kusimama kwaajili ya Nyerere. Afrika inatakiwa kukumbushwa wajibu iliomtupia mtu huyu, mzigo wa kuendesha vuguvugu zote za ukombozi,” alisema. “Mwisho wa siku, hakuna hata mmoja anayesema Tanzania ilistahili japo kutajwa tu kwa kufanikisha mission hii, mission ya kuwa nasi kama marafiki, mission ya kutufanya tuendeshe vuguvugu za ukombozi wa Afrika. Wote tulienda kwa njia tofauti, kwa sura tofauti hadi Tanzania kukomboa nchi zetu na hatujaenda tena Tanzania. Well, naenda kuwa mwenyekiti wa AU, ntashughulikia suala hili,” alisema.
“Hakuna aliyetambua kile Nyerere alichokifanya. Sisi wa Wazimbabwe sio wachoyo wa shukrani, ni taifa lenye shukrani na tutamuenzi mtu huyu.”