NEWS

29 Aprili 2019

Makundi ya WhatsApp Yaijazia yanga Manoti


Kuelekea mchezo wa Ligi Kuu Tanzania bara hii leo kati ya Yanga na Azam FC, umoja wa makundi ya Whatsapp ya klabu ya Yanga umewachangia wachezaji wao ili kuchagiza ushindi katika mchezo huo.

Umoja huo umechangia kiasi cha 1.5 milioni kwa wachezaji ili kuhamasisha ushindi katika mchezo huo na kuahidi kuwa watarudi tena katika michezo mingine inayofuata kuelekea mwishoni mwa msimu.

Kiasi hicho cha pesa kimetolewa katika mazoezi ya timu hiyo jana, April 28, katika uwanja wa Uhuru, ambapo Mwenyekiti wa umoja huo amesema, "tumekuwa tukikutana mara kwa mara, japo hapa katikati hatujaonana, leo tumerudi tena kuelekea mechi yetu ya kesho (leo) dhidi ya Azam na tutarudi tena kwenye mechi yetu ya FA dhidi ya Lipuli".

Naye Mhazini wa umoja huo amesema, "sisi tumekuja na pesa kidogo japo siyo nyingi lakini angalau tunaonesha tu moyo kuwa tupo pamoja. Leo tumekuja na milioni moja na nusu ambayo itawasidia japo vocha, nauli au matumizi mengine".

Pia Meneja wa Yanga, Nadir Haroub Cannavaro alionekana katika tukio hilo. Ikumbukwe kuwa kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera alikuwa katika hali ya kutokuwa na maelewano mazuri na meneja huyo baada ya kumtuhumu kutumiwa na Simba kuihujumu klabu yake kabla ya mchezo wa mzunguko wa pili uliozikutanisha timu hizo.

Yanga na Azam FC zinatarajia kuvaana, saa 10:00 jioni ya leo katika Uwanja wa Uhuru. Yanga bado inaongoza ligi ikiwa na alama 74, huku nafasi ya pili ikishikiliwa na Simba yenye alama 69 na Azam FC ikiwa katika nafasi ya tatu kwa alama 66.