NEWS

17 Novemba 2019

Biteko Ang’aka Kuhusu Mishahara ya Watanzania Migodini Na Issa Mtuwa – Geita

Waziri wa Madini Doto Biteko pamoja na kuupongeza uongozi wa mgodi wa dhahabu wa Geita “GGM” katika  mambo mengi leo tarehe 16/11/2019 alikuwa “mbogo” kwa uongozi huo kuhusu suala la mishahara wanayolipwa Watanzania ambapo amebaini kutokuwepo kwa usawa. 
 
Biteko amesema anaumizwa sana na jambo la malipo ya mishahara kati ya Watanzania na wageni licha ya kulingana kwa sifa, ujuzi na elimu na wakati mwingine mtazania anasifa zaidi kuliko mgeni lakini bado mtanzania analipwa chini kuliko yule mgeni.  

Kutokana na hali hiyo, Biteko ameuagiza uongozi wa GGM kuwasilisha orodha ya malipo ya mishahara ya wafanyakazi wote (Payroll) kwa Kamishna wa Madini Mhandisi David Mulabwa wiki ijayo. Biteko alianza kuhoji idadi ya idara zilizopo na zinaongozwa na akina nani huku akiuliza kuna watu wangapi wa kigeni katika idara hizo na majukumu yako.  

“Sheria ya madini hasa sheria ya Local content inatoa muongozo ni namna gani na wakati gani mgodi unaweza kumuajiri mtaalamu wa fani fulani kutoka nje endapo hakuna mtanzania wa kuweza kushika wadhifa huo” amesema Biteko.  

Ameongea hayo wakati akiongea na uongozi wa mgodi wa GGM mkoani geita alipotembelea mgodini hapo kwa ziara maalum ya kikazi kwa lengo la kufuatilia na kukagua uendeshaji wa shughuli za mgodi huo, ufuatilia na kuangalia utekelezaji wa malalamiko ya wananchi na malipo ya ushuru wa Halmashauri (Service Levy) ambapo mgodi huo unawajibika katika malipo hayo. 

Aidha, Biteko amekwenda kujiridhishi katika masuala mbalimbali ambayo kamati maalumu aliyoiunda kwenda mgodini hapo kwa ajili ya kuangalia na kukagua ili ajiridhishe kabla ya kutoa idhini ya kuruhusu mgodi huo kuanza uchimbaji wa chini kwa chini (Underground) kufuatia maombi ya mgodi huo kwa waziri. 

Kwa mujibu wa kifungu cha 40 cha marekebisho ya sheria ya madini ya mwaka 2017  hairuhusu uchimbaji wa chini kwa chini kwa mwekezaji au mgodi mpaka apate idhini (Kibali) ya waziri mwenye dhamana ya Madini ambapo Waziri alianisha mambo mengi ya kuzingatiwa na mgodi kabla hawajaruhusiwa. 

Biteko ameendelea kusisitiza kauli yake ya mara kwa mara kuwa raslimali hizi ziwe neema kwa wananchi na sio mateso. Kauli hiyo ameitoa kufuatia malalamiko ya wananchi wapatao 350 ambao makazi yao yalipitiwa na tetemeko wakati wa milipuko mbalimbali mgodini hapo wakati wa ulipuaji wa miamba. 

Ameongeza kuwa hadi kufikia mwisho mwaka huu ukurasa wa suala la malipo ya fidia ya suala hili liwe limefungwa na kwamba wenye malalamiko wote wapeleke kwa Mkuu wa Wilaya Geita kuanzia tarehe 18-23/11/2019. 

Kwa upande wa uongozi wa mgodi ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Mgodi Richard  Jordanson na Makamu Mkurugenzi Mtendaji Simon Shayo kwa nyakati tofauti wametoa shukrani kwa ujio wa Waziri kwenye mgodi wao ikiwa ni mara yake ya kwanza kutembelea tangu alipoteuliwa kuwa Waziri wa Madini.  

Wameongeza kuwa mgodi wao upo mstari wa mbele kutekeleza maagizo ya serikali na kwamba wanapenda kuwa msistari mbele na wawe wa kwanza katika kuchangia sehemu kubwa itakayo changia pato (GDP) la taifa kwa upande wa madini. 

Shayo amemwambia waziri kuwa mambo mengi aliyoyasema Waziri kama vile; mpango wa ufukiaji mashimo baada ya mgodi kufungwa, ulipaji wa ushuru wa Halmashauri za wilaya (Service levy), mchakato wa ulipaji wa fidia ya wananchi na utekelezaji wa sheria ya local content vinatekelezwa baadhi vimeshakamilishwa na baadhi vipo kwenye taratibu za kukamishwa.  

Akiwa kwenye mgodi wa RZ unaomilikiwa na mwekezaji kutoka china anae fahamika kwa jina la “Lyuu” amemtaka mwekezaji huyo kwa kufanya kazi zake kwa kuzingatia sheria zote zikiwemo za madini, kazi na utoaji wa mikataba ya ajira na makato ya NSSF kwa wafanyakazi wake na kuiwasilisha kwa mamlaka husika.  

“Lyuu” amesema ameshukuru waziri kutembelea mgodi kwake na amepokea maelekezo ambayo ameyakubali na kuahidi kuyatekeleza. Wakati wakati huo huo wafanayakazi walipo mgodini hapo amewataka kuwa waaminifu na kuepuka vitendo vihovu kwa mwekezaji.