NEWS

12 Machi 2021

Mganga Mkuu Wa Serikali Avitaka Vyuo Vikuu Vya Afya Nchini Kuboresha Maadili Ya Wahitimu.


Na WAMJW- DSM
MGANGA MKUU wa Serikali Prof. Abel Makubi ameagiza uongozi wa chuo Kikuu cha Afya na Sayansi shirikishi Muhimbili (MUHAS) ni vingine inchini, kuboresha suala la maadili kwa wanafunzi wanaopita katika vyuo vya Afya ikiwemo suala la matumizi ya lugha na mavazi pindi wawapo maeneo yote ya utoaji huduma za afya.

Prof. Makubi ameyasema hayo wakati akiongea na uongozi wa chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili, pindi alipofanya ziara ya kujionea shughuli zinazoendelea katika chuo hicho ikiwemo utafiti wa miti dawa itayosaidia kupambana dhidi ya magonjwa yakuambukiza na yasiyoambukiza nchini.

“Imefika mahali ambapo maadili ya baadhi ya wanafunzi wetu ambao wanamaliza vyuo vikuu alafu wanakuja kufanya kazi kwenye mahospitali yamekuwa changamoto za kitabia, kukosa heshima,uvaaji na kukosa nidhamu ya kazi, na ndiyo maana nimeomba wasajili wawe hapa ili kuonesha msisitizo suala la maadili, tusiishie wanafunze ambao wamemaliza” amesema.

Ameendelea kusema kuwa, ifike muda tutengeneze mwongozo wetu wa jinsi ya kuvaa na matumizi ya lugha, nidhamu ya kuwajibika na tabia hii itasaidia kuboresha maadili mbele ya kila mtu pasi kuangalia rika au jinsia katika maeneo ya kutolea huduma za Afya.

Serikali imekuwa ikipokea malalamiko mengi sana kuhusiana na tatizo la maadili linalofanywa na baadhi ya Watumishi wetu wachache jambo ambalo ni kinyume na taaluma zetu katika utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Aidha, Prof. Makubi amewataka Wataalamu hususan Waalimu wa chuo hicho kutumia taaluma zao kwa kujitokeza katika katika jamii ili kutoa elimu kuhusu njia za kujikinga dhidi ya magonjwa yakuambukiza na yasiyoambukiza ili kuijenga jamii yenye afya bora.

Sambamba na hayo, Mganga Mku wa Serikali imeviagiiza vyuo vikuu vya Afya kuangalia namna ya kutilia mkazo somo wa Uongozi, Uwajibikaji na Utawala kwa watumishi wa sekta afya ambao baadae ndiyo wanaweza kuwa Waganga wakuu wa Wilaya, Mikoa na Wafawidhi wa Hospitali. Suala la “Health Governance kwa maana ya “Leadership and accountability” ni kipaumbele cha Kisera kwa Mwaka huu baada ya kugundua baadhi ya taasisi na Hospitali zinakwana kwa sababu ya uongozi usiojitambua, osiowajibika , usio na matokeo (maendeleo), uzalendo na kukosa umoja miongoni mwa watumishi.

Licha ya Serikali kutoa udhamini kwa Wataalamu wa Afya zaidi ya 319 ndani ya nchi ,ambao umegharimu TZS billion 3.3, Prof. Makubi ameweka wazi kuwa Serikali itaendelea kutoa udhamini kwa Wataalamu hao ili kuboresha huduma kwa wananchi kwa kutoa huduma za kibingwa ndani ya nchi, na kupunguza gharama za matibabu ambazo zingetumika kwa matibabu ya nje ya nchi.

“Serikali mwaka huu tumetoa udhamini za Wataalamu wanaofika 319 ndani ya nchi na wengine nje ya nchi, ni namba kubwa na nikujitoa sana kwa Serikali kuhakikisha kwamba kunakuwa na madaktari Bingwa wakutosha katika maeneo yote Madaktari, Wauguzi, Wataalamu wa Maabara, Wafamasia na sehemu nyingine” amesema