NEWS

30 Aprili 2019

DC na muuza madafu watoleana Bastola na Panga kisa vitambulisho vya Magufuli

Mkuu wa Wilaya Nanyumbu, Moses Machali, amedai kunusurika kukatwa panga na muuza madafu akihamasisha wajasiriamali kuchukua vitambulisho vya Wafanya biashara wadogo wadogo.



Machali amethibitisha taarifa hiyo inayoeleza kuwa baada ya kufika katika kijijini cha Mikangaula wilayani humo, alisimama kununua madafu huku akikagua wenye vitambulisho na kuhamasisha wasio navyo kulipia lakini mmoja wa wauza madafu alianza kukashifu Serikali akisema inawaibia wananchi.

“Ni kweli ilitokea, nilienda kutoa taarifa jana (Juzi) katika Kituo cha Polisi cha Mangaka wilayani hapa, kwa hiyo siwezi kuzungumzia kwa kina liko chini ya uchunguzi,” ameeleza DC Machali kwenye mahojiano yake na gazeti la Mwananchi.

Tayari Polisi mkoani Mtwara wameshatolea maelezo juu ya tukio hilo, ambapo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Blasius Chatanda, amesema taarifa alizopata kutoka eneo la tukio hilo ni kwamba baada ya kutofautiana kauli na kijana huyo muuza madafu, DC Machali alitoa bastola kumtishia.

“Niko safarini Morogoro. Hata hivyo, taarifa za awali nilizozipata ni kwamba yeye (DC) alimtolea bastola muuza madafu baada ya kupishana lugha, sasa mazingira ya kutoa hiyo bastola sijui lakini mpigie msaidizi wangu ofisini atakupa taarifa za kina, ”amesema Chatanda.

Akielezea kwa undani juu ya sakata hilo, DC Machali amesema katika hali ya kustaajabisha muuza madafu huyo mkazi wa Msufini alianza kutoa maneno ya kuikashfu Serikali ya wamu ya tano.