NEWS

28 Novemba 2019

Irene Uwoya Awaomba Wasanii Kufanya Jambo Hili


Muigizaji wa filamu za Bongo, Irene Uwoya, amewaomba wasanii wenzake kutenga muda wa kukumbuka familia zilizoachwa na wasanii wenzao, ambao wametangulia mbele za haki.


Uwoya ameandika hayo kupitia ukurasa wake wa Instagram, baada ya baadhi ya wasanii wa filamu kwenda mkoani Tanga na kufanya Dua ya kumrehemu, aliyewahi kuwa msanii wa nyimbo na vichekesho Marehemu Sharo milionea.

"Kwanza kabisa nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa wasaniii wote walioshiriki kwenye kumbukumbu ya ndugu yetu Sharo, najua tuna majukumu mengi, kila mtu ana maisha na mipango yake, pia najua sio lazima kuwasiliana au kusaidia familia za wenzetu waliotangulia ila inahitaji moyo tu wakujitolea" ameandika Irene Uwoya.

Aidha Uwoya ameongeza kuwa, "Naomba wasaniii wenzangu, hawa ndugu zetu walio tangulia na kuacha familia nyuma, tujitahidi kwa dakika chache kuwajulia hali, wao wanajitahidi kupambana na maisha ili wasilale njaa angalau familia zao ziishi, wengine wanaishia njiani katika harakati zao na kuacha familia kwenye wakati mgumu kwa sababu wao ndo ilikuwa tegemeo lao"ameongeza.

Uwoya aliendelea kwa kusema kuwa, "Mfano mimi Marehemu sharo sikuwahi kumjua wala kumuona kwa sura, lakini nimekutana na mama yake kwenye mazingira ya ajabu sana ambayo sielewi lakini naamini Mungu alipanga iwe hivyo".