NEWS

24 Novemba 2019

Marekani yataka makampuni ya mitandao ya kijamii kuzifuta akaunti za viongozi wa serikali ya Iran

Marekani imeyataka makampuni ya Facebook, Instagram na Twitter kuzifuta akaunti za viongozi wa serikali ya Iran hadi pale nchi hiyo itakaporejesha mtandao wa intaneti nchi nzima. 

Iran imezima intaneti nchi nzima kwa zaidi ya wiki moja katikati mwa ghasia zilizotokana na maandamano. 

Mwakilishi maalum wa Marekani nchini Iran, Brian Hook amesema utawala wa Tehran umejaa unafiki kwasababu wanazima intaneti lakini serikali inaendelea kuitumia mitandao. 

Amesema wameyataka makampuni hayo matatu kuzifunga akaunti za viongozi wa juu akiwemo Ayatollah Khamenei, waziri wa mambo ya nje Zarif Javad na rais Hassan Rouhan, hadi pale watakaporejesha intaneti. 

Maandamano yaliibuka Novemba 15 nchini Iran, saa chache baada ya tangazo la kupanda kwa bei ya mafuta. Siku iliyofuata serikali ilizima intaneti katika hatua ya kuzuia usambazaji wa vidio za maandamano.